JITAFUTE


JITAFUTE

10th March 2018

By Pastor Sam Gripper

“Kwakuwa mtu atakaye kuiponya nafsi yake ataiangamiza, na mtu atakayeiangamiza nafsi yake kwaajili yangu ndiye atakaye isalimisha. Kwakuwa yamfaa nini mtu kuupata ulimwengu wote, kama akajiangamiza, au kujipoteza mwenyewe?”

LUKA 9:24-25

Kikubwa nitakacho andika siku ya leo kwa msaada wa Mungu, ni sababu inayoweza kumfanya mtu kujikuta katika point ya kujiangamiza na kujipoteza mwenyewe na namna ambavyo anaweza akajitafuta ili kurudi katika mpango wa Mungu.

Jambo la kwanza na la msingi ambalo nataka kulizungumzia hapa ni kwamba, kitu chochote katika maisha yako ambacho umekipa nafasi ya kukutafsiri, kitu hicho kina nafasi kubwa sana ya kuelezea uelekeo wako. Mara nyingi tumeviangalia vitu ambavyo havijabeba maana ya jinsi tulivyo na tukahisi ndiyo vitu vinavyotafsiri namna tulivyo, tukaviacha vitutafsiri, na  vikatupeleka katika point ya kujipoteza huku tukidhani kuwa tumejikamilisha katika hivyo.

“Msisumbuke, basi, mkisema, Tule nini? Au tunywe nini? Au tuvae nini? Kwa maana hayo yote mataifa huyatafuta; kwa sababu Baba yenu wa mbinguni anajua ya kuwa mnahitaji hayo yote. Basi utafuteni kwanza ufalme wake na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa”

MATHAYO 6:31-33

Mahitaji ya kimwili, ni moja kati ya vitu ambavyo tumehisi vinatafsiri jinsi tulivyo na tukavipa nafasi ya pekee sana, na mwishowe vinatupeleka katika kujipoteza. Katika kitabu cha Mathayo hapo juu, Yesu anataka tupate ufahamu wa kujua ni nini kinacho tutofautisha na mataifa (watu wasiomjua Mungu/kwa mazingira ya andiko hili, ni watu wasio Waisrael).

Kila mwanadamu, awe ameokoka au hajaokoka, yapo mambo anayoyahitaji. Utofauti wetu kama wana wa Mungu na watu ambao bado hawajamjua Mungu, unatakiwa kuwa katika namna tunavyoyatazama mahitaji yetu (mtazamo wetu kwa mahitaji yetu) na namna tunavyopiga hatua za kuyafikia.

Watu wasioijua kanuni ya Ufalme, wanatafuta mahitaji, lakini tunaoijua na kuiishi kanuni ya Ufalme, tunautafuta ufalme, maana hatuenendi kwa jinsi ya kuona lakini kwa jinsi ya Imani, na jambo kuu tunaloamini ni kwamba Mungu anajua yote tunayoyahitaji na anaweza kutupatia kwa ukamilifu, hivyo hatutendi wala kuenenda kwa hofu.

Mara zote tunajipoteza wenyewe ndani ya vitu ambavyo tumevitengeneza kwa mikono yetu wenyewe. Vitu vinavyozaa hofu na mashaka ya kujiona kila siku kuwa hatujakamilishwa na tunahitaji kujikamilisha kwa jitihada zetu binafsi.

Katika Mwanzo sura ya 11, Mungu aliweza kuona jaribio la watu wale kujifanyia mnara ni jaribio la kuwapeleka upotevuni, kwasababu ni jambo lililokuwa matokeo ya jitihada zao za kutaka kujijengea namna ya kuwatafsiri na kuwatambulisha kwa mafikio yao. Na jambo hili, likatafsiri ueleke wao.

Mahali ambapo tunauhakika wa kutojipoteza ndani ya mambo tunayoyahitaji, sio mahali tunapohitaji kujipatia uhuru wa kushughulika na mambo hayo kwa nguvu zetu binafsi, lakini ni mahali ambapo tutatafuta na kuuona ukamilifu wa mambo tunayoyahitaji yakitokana na nguvu zetu za kuutafuta kwanza Ufalme wa Mungu.

Kuwa na nguvu ya kumtafuta Mungu badala ya mahitaji, haimaanishi tusijihusishe na shughuli yoyote ya uzalishaji na tuanze kushinda makanisani. Lakini inamaana kuwa katika kila tulifanyalo, lazima tuwe na uhakika kuwa tupo na tunaishi ndani ya kanuni za Ufalme. Adamu ndani ya bustani ya Edeni, alikamilishwa katika kila kitu kwakuwa kila alichokihitaji na kukifanya, alikipata na kukifanya akiwa ndani ya uwepo wa Mungu.

Sio unayoyahitaji ndiyo hutafsiri wewe ni nani, lakini ni vile ulivyojiwekeza katika Ufalme wa Mungu ndiyo hukutafsiri wewe ni nani.

“Kwa sababu hiyo nawaambieni, Msisumbukie maisha yenu, mle nini au mnywe nini, wala miili yenu mvae nini. Maisha je, si zaidi ya chakula, na mwili zaidi ya mavazi?”

MATHAYO 6:25

“Akawaambia, Angalieni, jilindeni na choyo, maana uzima wa mtu haumo katika wingi wa vitu vyake alivyonavyo.”

LUKA 12:15

#Jitafute

© Pastor Sam Gripper

TAG PENUEL LUHANGA/TOTAL TRANSFORMATION

grippersamuel@gmail.com
Unknown
Unknown

This is a short biography of the post author. Maecenas nec odio et ante tincidunt tempus donec vitae sapien ut libero venenatis faucibus nullam quis ante maecenas nec odio et ante tincidunt tempus donec.

No comments:

Post a Comment