KUISHINDA HATIA




KUISHINDA HATIA

21ST JANUARY 2018
Pastor Sam Gripper
UTANGULIZI
Kupitia utafiti wangu mdogo na usio rasmi sana, lipo jambo niligundua kuhusu hatia. Hatia, ni jambo pekee ambalo linaweza likaishi na mtu kwa muda mrefu sana hata kama kosa ambalo huyo mtu alilifanya lilifanyika mara moja tuu tena miaka kadhaa iliyopita.
Hii inanipeleka katika point ambayo natakiwa kuamini kuwa sababu pekee ya watu wengi kuhisi hawana nguvu wala uwezo wa kuishi maisha matakatifu, au kujiona wao ni wa dhambi na hakuna point Mungu anaweza akawakubali, si kwasababu ya dhambi walizozitenda lakini ni kwasababu ya hatia ambazo dhambi walizozitenda zinaiazalisha ndani yao na kutafsiri kila hatua ya maisha yao.
Iko point ambayo dhambi na hatia hukutana. Kwa tafsiri rahisi, dhambi ni kukosea shabaha, au kutenda chini ya kiwango/viwango vilivyokusudiwa. Hatia huzaliwa pale ambapo mtu hutakiwa kuwajibika kulingana na kukosea kwake shabaha au kuishi na kutenda chini ya viwango vilivyo kusudiwa.
Hatia ni hisia mbaya sana na huambatana na maumivu makubwa mno ambayo kimsingi huweza hata kugharimu maisha ya mtu. Kama hatutajua namna ya kushughulika na hatia zinazozalishwa ndani yetu kwa sababu ya makosa mbalimbali, tutakuwa tupo mahali pa hatari sana.
Kila mtu huwa kuna mahali anakosea, na kutokana na kosa husika hukumbana na hali hii ya kushambuliwa na hatia. Si ajabu hata baadhi watu waliookoka wakawa wanapitia hali hii pia.
Somo hili kwa msaada wa Roho Mtakatifu, ni hatua ya kutufungua fahamu zetu juu ya kushughulika na hatia zetu na kutufanya tuuishi na kuufurahia uhuru ndani ya Kristo
MAANA YA HATIA
Nikiwa nipo chekechea zamani sana, niliwahi ku experience namna hatia inavyotesa na hata ninapoongozwa kukuletea somo hili, naelewa hasa ni nini nakizungumzia na kwa upana gani natakiwa nikizungumzie. Naweza kusema kama mtoto, kwangu mimi ndiyo ilikuwa mara ya kwanza nayahisi maumivu haya ya hatia.
Siku moja nikiwa na rafiki zangu tukiwa njiani kutoka shuleni, nilijikuta natamani sana bagia. Na kwakuwa nilikuwa tayari nimeitumia hela yangu yote wakati wa mapumziko, sikuweza kununua. Nilipofika nyumbani, nilikuta mama ndiyo kwanza anawasha moto ili apike chakula cha mchana.
Kwakuwa nilikuwa naelewa wapi mama huwa anaweka hela, niliingia moja kwa moja hadi chumbani kwake na kuchukua shilingi hamsini kisha nikarudi shuleni (kwakuwa hapakuwa mbali sana na nyumbani), kuzifuata zile bagia. Nilinunua za kutosha, na nikawagawia baadhi ya rafiki zangu pia.
Niliporudi nyumbani, nilikuta chakula tayari kipo mezani na mama na kaka yangu tuliyefuatana kuzaliwa wameshaanza kula muda mchache tuu. Nilipokata tonge la ugali na kutoweza katika ile mboga, nilihisi inamapungufu makubwa sana, ingawa sikuwa najua sana kuhusu mapishi lakini niliweza kuhisi. Na kikawaida, nilikuwa mwepesi sana kulalamika pale kinapopikwa chakula nisichokipenda au pale chakula kinapopikwa katika namna nisiyoipenda.
Dakika hii, kabla sijaanza kulalamika, nikakuta mama ndiyo anakuwa wa kwanza kuongea. Hakuongea maneno mengi, yalikuwa machache lakini yaliuchoma moyo wangu kwa hatia kuu. “Mmeona, tunakula mboga ambayo haina kitunguu kwasababu mmoja wenu aliingia chumbani na akachukua hela ambayo ilitakiwa tununulie kitunguu. Sasa ametufanya tule mboga isiyo na kitunguu.”
Naamini mama alijua kuwa nimechukua ile hela, na hakukosa hela ya kununulia kitunguu, lakini alitaka anifundishe jambo kubwa. Sikuwa na nguvu ya kuadmit kuwa ni mimi, lakini niliumia kiasi kilichofanya nijione nimekuwa na hatia. Nikadhamiria, kesho yake nitakapopewa hela ya shule, nitairudisha mahali nilipoichukua ile nyingine. Nilijikuta naumia sana. Nikafanya hivyo.
Hatia inaelezewa
Hatia ni hisia inayokuleta katika point ya kuwajibika kutokana na ukosefu au kosa ulilolitenda. Hisia hii inaweza kutokana na kufanya jambo ambalo ni katazo au kushindwa kufanya jambo lililokuwa likihitajika lifanyike.
Na kimsingi ni kwamba, tunakutana na kuingia katika hatia kwasababu tumezungukwa na sheria na taratibu nyingi ambazo zipo kutuongoza katika njia njema ya maadili. Tunaposhindwa kuzitimiza, au tunaposhindwa kuzifuata, tunajikuta katika point ambayo tunatakiwa tuwajibike kwa yale tuliyotenda au tuliyoshindwa kuyatenda.
Hatia, ni hisia pekee ambayo itakutesa hata kama wengine hawajui kosa au dhambi uliyoifanya. Na ndio maana tupo na watu wengi makanisani, mashuleni na maeneo mbalimbali ya shughuli za kila siku, ambao kutoka kwao, tunaweza tusione makosa au mapungufu yoyote na tukahisi ni wakamilifu sana, lakini ndani yao panaweza kuwa na mzigo huu wa hatia juu ya mambo flani flani waliyowahi kuyafanya au wanayoyafanya.
Na kwasababu hatia ni mzigo unaoambatana na maumivu, kujichukia, kujilaumu nk. Wengi mara baada ya kukosa hujaribu sana kuficha dhambi au makosa yao huku wakiendelea kujichukia au hulaumu hali au mazingira ambayo yaliwafanya kuingia katika aina hizo za makosa. Hivyo kadri wanavyolaumu wengine au mazingira au kadri wanavyojitahidi sana kuficha makosa yao, wanahisi mzigo wa hatia ndani yao hupungua, lakini kimsingi, sio kweli.
“Adamu akasema, Huyo mwanamke uliyenipa awe pamoja name ndiye aliyenipa matunda ya mti huo nikala.”
MWANZO 3:12
Hii ni tabia ya wanadamu wote. Ni wachache sana ambao katika kukosa, watakubali kuuvaa wajibu wa kukubali kuwa wao ndio chanzo cha makosa, mapungufu na maharibifu. Lakini wengi, watasingizia mazingira, watasingizia au hali zozote ili kuukwepa mzigo huu wa hatia ndani yao, lakini kimsingi haukwepeki katika namna hiyo.
MTU, DHAMIRI NA ROHO MTAKATIFU
Asilimia kubwa ya watu ambao kutoka kwao mataifa (watu ambao bado hawajamjua Mungu) walitegemea kuwa watapata msaada wa kiroho ndiyo watu ambao wanaishi maisha ya kushindwa (defeated life) na kushtakiwa kila mara kwa sababu ya yale waliyowahi kuyatenda au wanayoyatenda.
Kwa sehemu tuu, niliwahi kupata nafasi ya kuzungumza na baadhi ya vijana wenzangu kadhaa ambao walinitafuta kibinafsi kabisa, (ni vijana wanaotumika kanisani) kunielezea ni kwa kiasi gani wamekuwa addicted na baadhi ya matendo au tabia zisizo faa na hawaoni namna ya kutoka katika vifungo hivyo.
 Katika hali ya utulivu kabisa ya kuzungumza nao juu ya hali hizo (maana na mimi pia nimewahi kupitia), nikagundua, asilimia kubwa (sio wote) ya watu ambao wanadhani wanateswa na aina flani ya tabia mbaya, dhambi au vifungo, katika namna halisi kabisa, huwa hawateswi na hizo dhambi lakini huteswa na mashtaka ya hizo dhambi.
Wengi ambao nimezungumza nao, huwa ninapenda kuwauliza hili swali, “Mara baada ya kujikuta umefanya hiyo dhambi, ulitubu?” Karibia wote hujibu ndiyo, kitu ambacho hunipeleka katika swali lingine, “Kama ni kweli ulitubu tena kwa kumaanisha, ni kwanini bado uendelee kushtakiwa na kushikiliwa katika kifungo ambacho tunaamini toba imekutoa?” Na kimsingi, huwa wanakosa majibu na kuniambia kila mara wanajikuta wana mzigo wa ile dhambi, na inafika point hadi wanajichukia.
Hivyo nataka tupate picha kuwa dhambi huweza kufanyika mara moja tuu, lakini hatia inayozalishwa kutokana na hiyo dhambi huweza kudumu milele kama tuu hatujajua namna Roho Mtakatifu anavyotenda katika Dhamiri zetu ili kutufunulia Upendo, Rehema na Neema ya Mungu kwetu.



Dhamiri
Kila mwanadamu anayo dhamiri. Na dhamiri ni moja kati ya vitu vinavyo akisi sura ya Mungu kwa mwanadamu, vingine ni utashi (uwezo wa kufanya machaguo na maamuzi), kuunda/kuumba na mengine mengi.
Dhamiri, ni uwezo au tabia ya asili (inayotokana na Mungu mwenyewe) inayotawala kiwango cha utakatifu wa mtu ili awe mtakatifu kama vile Mungu alivyo mtakatifu. Unaweza kuwa huijui dini yoyote, huna maadili yoyote ya kijamii, lakini kuna kitu ukifanya, ndani ya moyo wako utaisikia hukumu kuwa jambo ulilolifanya halikuwa sahihi. Ndivyo ambavyo dhamiri hufanya kazi.
Hivyo, wakati utashi unampa uhuru mwanadamu juu ya kufanya machaguo na maamuzi mbalimbali, dhamiri inamuwajibisha au kumshuhudia wanadamu juu ya maamuzi aliyoyafanya kama ni halali ama si halali.
“Kwa kuwa wote waliokosa pasipo sheria watapotea pasipo sheria, na wote waliokosa, wenye sheria, watahukumiwa kwa sheria. Kwa sababu, sio wale waisikiao sgeria walio wenye haki mbele za Mungu, bali ni wale waitendao sheria watakaohesabiwa haki.
Kwa maana watu wa mataifa wasio na sheria wafanyapo kwa tabia zao yaliyo ndani ya torati, hao wasio na sheria wamekuwa sheria kwa nafsi zao wenyewe. Hao waionyesha kazi ya torati iliyoandikwa mioyoni mwao, dhamiri yao ikiwashuhudia, na mawazo yao wenyewe kwa yenyewe, yakiwashtaki au kuwatetea.”
WARUMI 2:12-15
Hivyo katika maandiko haya, Paul anajaribu kuonesha kuwa hapana upendeleo mbele za Mungu, kila mtu atahukumiwa kulingana na matendo yake. Wayahudi kwakuwa walikuwa na sheria/Torati walitakiwa kuhukumiwa kwa hiyo, na watu wa mataifa ambao hawakupewa kuongozwa na torati, watahukumiwa kwa dhamiri zao.

Hivyo Mungu alidhamiria kuwa dhamiri iwe ni alama au jambo litakalo muongoza mwanadamu katika utakatifu wote wa Mungu. Ndio maana tunapokosea, dhamiri zetu hutuambia kuwa hapa tumekosea na hutuacha katika point ya kuhukumiwa na makosa tuliyoyafanya. Kwa lugha nyingine maana yake, dhamiri zetu huzaa hatia mara baada ya sisi kuingia katika kutenda kosa flani.
Mapungufu au athari ya dhamiri
Sio tuu kwa  dhamiri, kiujumla anguko la mwanadamu, liliathiri sura nzima ya Mungu kwa mtu. Hivyo kuanzia utashi, dhamiri na mengine yote ambayo yalikuwa yakiakisi sura ya Mungu kwa mtu yaliathiriwa. Na ndio kuanzia point hii, mtu hakutakiwa kuitegemea akili wala mawazo yake katika kumpendeza Mungu maana anguko/dhambi lilitia athari sura ya Mungu kwa mtu.
MWANZO 8:21c “Maana mawazo ya moyo wa mwanadamu ni mabaya tangu ujana wake;
Kwakuwa tayari anguko/dhambi imezitia giza dhamiri zetu hii huweza kupelekea mtu kuwaza kuwa jema ni baya na baya ni jema. Yohana 16:2-3, “Watawatenga na masinagogi; naam, saa yaja atakapodhania kila mtu awuaye ya kuwa anamtolea Mungu ibada. Na hayo watayatenda kwasababu hawakumjua Babab wala mimi”. Au kwa namna nyingine ningeweza kusema, watayatenda kwasababu sura ya Mungu haipo tena ndani yao.
Hivyo, mara baada ya anguko la mwanadamu katika bustani ya Edeni, mwanadamu anatakiwa kutembea katika namna ambayo hatakiwi kabisa kuyaamini hata mawazo yake mwenyewe maana yanaweza kumpeleka katika upotevu.
Hivyo katika uumbaji wa pili ambao Mungu anaufanya katika Roho Mtakatifu, anakusudia kutupa Roho Mtakatifu ili awe si tuu mbadala wa dhamiri zetu, lakini awe na atende zaidi ya dhamiri zetu zilivyokuwa zikitenda. Ukikosa umakini, unaweza kuhisi kazi ya dhamiri na Roho Mtakatifu ni sawa. Lakini katika somo hili nitakuonesha utofauti mkubwa sana kwa msaada wa Roho Mtakatifu.

Roho Mtakatifu
“Naye akiisha kuja, hyo atauhakikishia ulimwengu kwa habari ya dhambi, na haki, na hukumu”
YOHANA 16:8
Kama dhamiri, Roho Mtakatifu yupo kutawala kiwango cha utakatifu wa mtu na kuhakikisha mtu anakuwa mtakatifu kama Mungu alivyo mtakatifu.
Lakini, zaidi ya dhamiri, yeye Roho Mtakatifu, ana uwanda mpana zaidi. Haiishii kukuonesha lipi ni baya na lipi ni jema na kukuachia hukumu moyoni, bali yeye hupiga hatua nyingine ya zaidi ya kukwambia namna unavyotakiwa kutenda ili kutoka chini ya hiyo hukumu, na zaidi kabisa hukuombea ili utoke chini ya hiyo hukumu.
“Kadhalika Roho naye hutusaidia udhaifu wetu, maana hatujui kumba itupasavyo; lakini Roho mwenyewe hutuombea kwa kuugua kusikoweza kutamkwa.”
WARUMI 8:26
Yohana 16:8 tulioiona hapo juu, inatueleza kuwa Roho Mtakatifu huuhakikishia ulimwengu kwa habari ya dhambi (kwa neno la kingereza, convict au prove), jambo linaloweza kumaanisha:-
·        Hufunua hatia ya ulimwengu/huutia ulimwengu hatiani
·        Humleta mtu katika point ambayo atakubali kuwa yeye ni mkosefu
·        Hutumia ushahidi kamili, kumtia mtu hatiani
Lakini, kinacho nifurahisha zaidi ni kwamba hufunua thamani ya mtu kwa Mungu, hata katika mazingira ambayo yanamfanya asione thamani yake na kukosa ujasiri wa kumsogelea Mungu kama Baba. Hivyo, Roho Mtakatifu, huwa mshauri wa kumuongoza mtu katika mashauri yote ya ki-Mungu.


NAMNA DHAMIRI NA ROHO MTAKATIFU VINAVYO SHUGHULIKA NA HATIA
AINA KUU MBILI ZA HATIA
1.     Hatia ya uongo
Kitabu cha Mathayo 27:1-10 kinaeleza kuhusu habari ya Yuda Iskariote na mwisho wa maisha yake. Yapo mambo kadhaa hapa natamani tuyaone:-
·        Ni kweli Yuda alitenda dhambi iliyozaa hatia ambayo ilimtesa hata mara baada ya siku aliyoitenda ile dhambi kupita
·        Hatia yake, aibu na hukumu ilielekezwa kwake mwenyewe na kumfanya aanze kujichukia, kujiona duni na kujiona hakuna aina ya msamaha anayoweza kuistahili
·        Hili lilipelekea ajiue
Ninapozugumza kuwa hatia hii inaitwa hatia ya uongo, wala simaanishi kabisa kuwa mhusika hakutenda dhambi husika na hatakiwi kuwajibishwa katika dhambi yake. Ninacho maanisha hapa ni kwamba, ni hatia ya uongo kwa sababu kuwajibishwa huku kunatokana na chanzo kisicho sahihi kufanya hivyo ambacho ni Dhamiri.
Nathubutu kusema, si chanzo sahihi, kwasababu badala ya kukuinua katika kuanguka kwako, kinazalisha chuki, hukumu na hasira juu yako mwenyewe kama ilivyotokea kwa Yuda
Katika Galatia 2:8-14, Paul anatuambia kuwa ilimpasa kumkemea Kefa (Petro kwa jina lingine), ambaye alikuwa anajua wazi kuwa msingi wa wokovu au neema ya Kristo haupo katika utaifa, lakini upo katika Imani. Paul anasema Petro alikuwa mnafiki, kwasababu alipokuwa akikutana na watu wa mataifa (wasio wa Israeli), aliweza kuchangamana nao vizuri na kufanya shughuli kadhaa wa kadha wakiwa pamoja, lakini aliposikia tuu watu wa Yakobo (Waisraeli) wanakuja, alijihukumu na kuacha kuchangamana nao, jambo ambalo Paul analiita ni unafiki.
Lakini hii ni kwasababu, Petro aliruhusu dhamiri/mawazo yake yaamue nini anatakiwa afanye. Kila mara tunapoziacha dhamiri zetu zishughulike na makosa yetu, lazima tujue kuwa huwa tunakuwa katika hali mbaya sana.
Ukweli kuhusu hatia ya Uongo
       I.            Huzalishwa ndani yetu kupitia dhamiri zetu na shetani huishikia bango ili tusipige hatua mpya
     II.            Ni hatia ya uongo kwasababu hukudanganya juu ya Mungu alivyo. Wengi wanaopitia katika hali hii ya kushtakiwa, wamefika hatua hata ya kumuona Mungu kuwa hana upendo, hataweza kusamehe na amechoshwa na madhaifu ya mtu kitu ambacho ni uongo mtupu.
  III.            Huifanya aibu, kudharauliwa, kuhukumiwa na kila baya, lielekezwe kwa mhusika na kumfanya mhusika aanze kujichukia yeye badala ya kuichukia dhambi.
“Kama mashariki ilivyo mbali na magharibi, ndivyo alivyoweka dhambi zetu mbali nasi”
ZABURI 103:12
“Atarejea na kutuhurumia, atayakanyaga maovu yetu, nao utazitupa dhambi zao zote katika vilindi vya bahari”
MIKA 7:19
“Kwasababu nitawasamehe maovu yao, na dhambi zao sitazikumbuka tena”
EBRANIA 8:12
“Hata imekuwa mtu akiwa ndani ya Kristo amekuwa kiumbe kipya, ya kale yamepita, tazama yamekuwa mapya”
2WAKORINTHO 5:17
Maandiko haya yote, yanaelezea ni kwa namna gani Mungu huitazama dhambi ambayo imekwisha kutubiwa tayari. Tendo la kuishi na hatia ya dhambi uliyoitenda miaka kadhaa iliyopita, ni maamuzi yako binafsi.
2.     Hatia ya Kweli
Hii ni hatia ya kweli kwasababu huzalishwa na chanzo sahihi ambacho ni Roho Mtakatifu, na ye eye hata mara baada ya kushuhudia kuwa u mkosaji, huwa hakuachi katika point hiyo hiyo uendelee kujihukumu. Yeye hukuinua na kukupeleka moja kwa moja kwa Mungu kama Baba yako na sio kama jemedari wa jeshi au hakimu.
Ukweli kuhusu hatia ya Kweli
       I.            Huzalishwa ndani yetu na Roho Mtakatifu, jambo linalo mkosesha shetani nafasi ya kuitumia kinyume nasi
     II.            Aibu, hukumu, kudharauliwa, na kila baya litokanalo nayo, huelekezwa kwa dhambi husika na kumfanya mtu aichukie dhambi na sio kujichukia yeye mwenyewe.
  III.            Kupitia hii, Roho Mtakatifu humuinua mtu huyu na kumfanya aione thamani yake na aone hakuna kosa lolote lililokubwa kuzidi wingi wa rehema, neema na upendo wa Mungu kwa mtu.
  IV.            Kupitia hii, Roho Mtakatifu hutuonesha kuwa tu wapekwe na hatuwezi kuendele maana tumetengwa na Baba na hutuonesha namna ya kumrudia
    V.            Kupitia hii, Roho Mtakatifu hutuongoza katika kweli yote
NIFANYE NINI NINAPOSHAMBULIWA NA HATIA YA UONGO
1.     Lazima uelewe kuwa, unashambuliwa na hatia ya uongo kwasababu ni kweli kuna mahali umekosea au ulikosea. Shetani ni mshtaki wetu, lakini hawezi akakushtaki kama hakuna mahali ulipolegeza viwango vya utakatifu na kumkosea Mungu.
2.     Wapo baadhi ya walimu na wachungaji wangekupa hatua ya kuingia katika maombi, lakini mimi naomba nikupe hatua muhimu sana kabla ya hiyo kuwa  JIPENDE. Usiruhusu kamwe chuki na kujiona duni ambako hatia ya uongo inakuletea kuwe ni sehemu ya maisha yako. Hata kama ni kweli umekosea na unarudia kosa hilo mara nyingi, siri ya kwanza ni kujipenda. Kadri unavyojipenda, utaitambua thamani yako, na hautaruhusu kamwe dhambi ishushe thamani yako. Ukijipenda, utaweza pia kujiombea.
3.     Fanya mipango na maamuzi ya kuamua kuiacha dhambi unayoifanya na kutengwa na hatia inayozaliwa. Hatua na mipango hii, ndiyo hasa huhitaji maombi ya kujitamkia kutengwa na hatia yako. Mruhusu Roho Mtakatifu akuongoze katika njia na namna atakayo wewe na sio vile mawazo vako yanakutuma
“Basi mwana akiwaweka huru, mtakuwa huru kwelikweli”
YOHANA 8:36
NATAMKA UHURU JUU YAKO KATIKA JINA LA YESU KRISTO










©Pastor Sam Gripper –
TAG PENUEL ASSISTANT PASTOR
TOTAL TRANSFORMATION ©2018
0657670972






















©Pastor Sam Gripper –


TAG PENUEL ASSISTANT PASTOR


TOTAL TRANSFORMATION ©2018


0657670972
Unknown
Unknown

This is a short biography of the post author. Maecenas nec odio et ante tincidunt tempus donec vitae sapien ut libero venenatis faucibus nullam quis ante maecenas nec odio et ante tincidunt tempus donec.

No comments:

Post a Comment