KUSUBIRI

THE WAIT – KUSUBIRI
January 14, 2018

UTANGULIZI
Kwa kawaida kabisa, hapana mtu ambaye anapenda kusubiri. Kila mtu hutamani kila anachokifanya au anachopanga kukifanya kifanyike ndani ya majira na wakati aliopanga tena kwa haraka.
Ukienda bombani kuchota maji, hautatamani ukute foleni, utatamani uchote na kuondoka, ukienda bank kufanya aina yoyote ya malipo, hutafurahia kukuta foleni ambayo itakufanya usubiri, ukienda kituo cha basi na basi lisipowasili katika muda uliotarajia, utajisikia vibaya na kukasirika kwakuwa unatakiwa kusubiri, unapopiga simu kwa rafiki yako, na ukakuta anaongea na simu nyingine na unatakiwa kusubiri lazima utakasirika tuu, unapopiga simu ya huduma kwa wateja na ukakuta mhudumu hapokei kwasababu anaongea na simu nyingine na unatakiwa kusubiri, ni wazi tuu utakasirika.
Hii yote ni kwasababu kusubiri ni jambo gumu sana lenye gharama ambalo mara nyingine hupima na kujaribu kiwango cha kuamini cha mtu. Na kiwango cha kuamini kinapopimwa au kujaribiwa, maana yake kiwango cha uwezekano wa kuwezekana au kutowezekana kwa mambo yanayotarajiwa au kusubiriwa kinapimwa na kujaribiwa pia.
“Hata watu walipoona ya kuwa Musa amekawia kushuka katika mlima, wakakusanyana wakamwendea Haruni, wakamwambia, Haya! Katufanyizie miungu itakayo kwenda mbele yetu, kwa maana Musa huyo aliyetutoa katika nchi ya Misri hatujui yaliyompata.”

KUTOKA 32:1
MUNGU HUTAKA TUSUBIRI KWA SABABU:
·        Ipo Ahadi 
Kimsingi, hapana kusubiri kama hapana ahadi inayotakiwa kusubiriwa. Mungu yupo na ahadi nyingi sana kwaajili yetu ambazo zimefunuliwa kupitia Neno lake. Kwa kukaa chini ya Neno lake, tunafanywa wangojezi kwa namna ya subira inayoleta tumaini na wamiliki wa ahadi hizo kabla hazijadhihirika, kwa njia ya imani. Hivyo, Mungu anataka tusubiri kwakuwa Ipo ahadi.
·        Yeye ndiye aliyeahidi
Kujua kuwa ipo ahadi, ni jambo la msingi na la thamani sana kwakuwa linatupa tumaini. Lakini kujua kuwa Mungu ndiye aliyeahidi hizo ahadi, ni jambo ambalo linatupa ujasiri wa kusimama thabiti katika kusubiri kwetu hata kama tutapita katika nyakati ngumu mno, kwasababu tuu ahadi zetu zimetoka katika chanzo chenye tabia ya uaminifu, ukweli na kutobadilika. Hivyo katika point hii, Mungu anatuinua kutoka katika kiwango cha kuitazama na kuisubiri ahadi hadi kiwango cha kumtazama na kumuangalia aliyeahidi na tabia zake.
“Nitakusujudu nikilikabili hekalu lako takatifu, Nitalishukuru jina lako, kwa ajili ya fadhili zako na uaminifu wako, kwa maana umeikuza ahadi yako, kuliko jina lako lote”
ZABURI 138:2
·        Ana nia na mpango thabiti juu ya kila anacho ahidi
Mara nyingi huwa napenda kuzungumza na rafiki zangu, kuwa Mungu hafanyi chochote anachokifanya kwasababu tuu ni Mungu, ni mamlaka iliyo kuu na hapana mamlaka yoyote ya kuuliza utendaji wake, bali nguvu inayomsukuma afanye chochote anachotaka kukifanya ni nguvu ya Kusudi.
Hapana jambo anafanya pasipo kuwa na kusudi. Mwanzo 1:26, anaeleza wazi juu ya mpango wake wa kumuumba mtu. Anasema atamuumba kwa sura na kwa mfano wake, tofauti kabisa na alivyo viumba viumbe vingine vyote. Na hii haituambii tuu juu ya aina ya mtu ambaye Mungu anakusudia kumfanya, lakini zaidi mpango juu ya aina ya maisha ambayo Mungu amekusudia mtu huyu aje kuyaishi.
Hivyo Mungu anaujua mpango wa ahadi yako vizuri kuliko wewe ujuavyo na yupo committed kuitimiza, pengine kuliko ambavyo wewe upo committed kuipokea, na pia alikuumba kutokana na ahadi aliyonayo juu yako. Kwa lugha nyingine, kabla ya wewe kuwepo ilikuwepo kwanza ahadi au kusudi, ambalo lilihitaji Mungu akuumbe hivyo ulivyo ili kufit katika kusudi/ahadi
·        Anafanya kazi zake katika majira na nyakati zake yeye mwenyewe.
Hii ni sababu nyingine ya muhimu ya kwanini Mungu anataka tuwe na tabia ya kumsubiri. Mwanzo 1:1, inaposema “Hapo mwanzo Mungu aliziumba mbingu na nchi, haimaanishi kuwa huu ndio ulikuwa mwanzo wake, lakini alikuwepo kabla ya wakati na anachokifanya hapa ni kuuanzisha wakati na kutuweka sisi chini/ndani ya wakati na majira husika.
Hivyo yeye anatuongoza katika nyakati zetu kwa kutawala mambo yaliyo nje ya nyakati zetu. Hivyo, tunatakiwa kumsubiri maana mambo tunayoyatarajia yapo nje ya nyakati zetu lakini ndani ya nyakati zake.
“Akawaambia, Si kazi yenu kujua nyakati wala majira, Baba aliyoyaweka katika mamlaka yake mwenyewe”
MDO 1:7
Sababu hizi za Mungu kutaka tutengeneze tabia ya kusubiri  ni sababu ambazo kimsingi zinatuchukua na kutuweka mahali ambapo tunajikuta ili kupokea ahadi zake, ni lazima tumtegemee kwa asilimia zote ili atende. Lakini mara nyingi tumekuwa na udhaifu wa kuziona sababu hizi zote kwamba zinatusaidia kumtegemea Mungu, badala yake tumekuwa na mitazamo ya tofauti juu ya sababu hizi.
MWANADAMU (KINYUME NA MUNGU) HUTAKA KUSUBIRI KWA SABABU:
·        Anajua ipo ahadi
·        Yupo na motives au nia binafsi juu ya ahadi tarajiwa
·        Ana wakati binafsi ambao anataka ahadi itimie
Katika mambo haya matatu hakuna mahali ambapo mwanadamu huweza au hutamani kuuona uaminifu wa Mungu kwa ukubwa kuliko ahadi tarajiwa. Ni katika point hii ambapo mwanadamu hushindwa kusema “Ahadi yangu itimie au isitimie kwa wakati niliotaka, bado Mungu ni mwaminifu, ahadi zake ni amini na kweli, na nitasubiri chini ya wakati wake ayadhihirishe mapenzi yake”
Na hii ni kwasababu anatarajia ahadi ya Mungu lakini anataka idhihirike kwa mapenzi yake binafsi na wakati wake ambao yeye (mwanadamu) anataka na sio Mungu. Na ndio maana sababu 4 za Mungu kutaka tuwe na tabia ya kusubiri ni tofauti na sababu zetu za kusubiri.
“Hata mwaomba, wala hampati kwasababu mwaomba vibaya, ili mvitumie kwa tama zenu”
YAKOBO 4:3
Nilipata kibali wakati Fulani, kutembelea mahali Fulani kwaajili ya kufanya huduma na nikabahatika kusikia shuhuda za nini Mungu aliwatendea watu wakati kipindi cha ushuhuda kinafanyika baada ya mimi kuhudumu.
Akasimama binti mmoja ambaye alitoa ushuhuda kuhusu uhitaji wa kaka yake kupata ajira, na vile ambavyo huyu binti alikuwa akifunga na kuomba mara kwa mara ili kumwomba Mungu kwaajili ya kaka yake. Katika maelezo yake huyu binti akasema, ilifika point ambayo yeye alichoka kuendelea kuomba na akamuwekea Mungu kile alichokiita yeye “deadline” kuwa hadi siku flani Mungu asipojibu, yeye hataombea hilo jambo tena.
Nilishtuka, kwasababu kwangu mimi kilikuwa ni kitu kigeni sana. Nikakumbuka wakati ambao Yesu alikuwa akiwafundisha wanafunzi wake kuomba, aliwapa maneno ya msingi sana “Utakalo lifanyike hapa duniani, lifanyike kama lifanyikavyo mbinguni”. Nikagundua kuwa huyu binti, alionesha tabia ambazo wanadamu wote huonesha. Kutafuta ahadi za Mungu huku tukimfunga atende katika nyakati zetu na kwa ukubwa ambao sisi tunauona.
Hivyo hata katika hali yetu hiyo ya ujinga Mungu anapotenda kwa sababu yeye yu mwaminifu, naweza kusema hutenda kama vile sisi tunavyotaka na sio vile yeye alivyokusudia. Hivyo kuziweka nyakati zetu na motives zetu katika ahadi za Mungu, ni sawa na kumzuia Mungu afanye kwa ukubwa aliokusudia yeye.

Wakati wowote, kiwango unachotakiwa kusubiri, kinapozidiwa na shauku yako binafsi ya kutaka ahadi idhihirike hata kabla wakati wa Mungu haujafika, Unashambuliwa na Tamaa

MWANZO 16:1-6, Inaeleza kuhusiana na kushindwa kusubiri kwa Sarai mkewe na Abram kunakofanya Sarai amruhusu Abram kuzaa na kijakazi, jambo ambalo linakuja kuwa mwiba kwa maisha ya Sarai na Abramu kabla ya mtoto kuzaliwa na hata mara baada ya mtoto kuzaliwa (Ishmael) na Yule mtoto wa ahadi (Isaka) anapokuja kuzaliwa.
Na sehemu kubwa ya uadui ambao upo hata hivi leo kati ya Waarabu na Waisrael, ni matokeo ya mtoto asiyekuwa wa ahadi (Ishmaeli) kuzaliwa kabla  ya mtoto wa ahadi (Isaka), kwasababu tuu wazazi walishindwa kusubiri.
“Kwa maana imeandikwa ya kuwa Ibrahimu alikuwa na wana wawili mmoja kwa mjakazi, na mmoja kwa mwungwana. Lakini Yule wa mjakazi alizaliwa kwa mwili, Yule wa mwungwana kwa ahadi”
GALATIA 4:22-23
MAMBO MAWILI YANAYOFANYA KUSUBIRI KUONEKANE NI KUREFU NA KUGUMU
1.     Uncertainty (kutokuwa na uhakika)
2.     Hofu ya kupoteza ahadi
Hebu fikiria, rafiki yako wa muda mrefu anapokupigia simu na kukwambia anakuletea zawadi ambayo hataki kuitaja ni nini. Katika hali hii, itakuwa ni ngumu sana kwako kumsubiri kwakuwa unashauku ya kutaka kujua anakuletea nini, na hata akikwambia umfuate popote alipo utakubali kwakuwa tuu, hujui amekuletea nini na ungetamani kujua. Hivyo utaona tuu ni kama muda hauendi hivi.
Jambo la ajabu ni hili, utakuwa na shauku sana ya kutaka kujua amekuletea nini kwasababu huna uhakika lakini utakuwa na hofu ya kuipoteza ahadi ya kitu usichokijua/usichokuwa na uhakika nacho.
Hivyo kikawaida, kusubiri kwetu huonekana ni kwa muda refu sana kwasababu tuu hatujui tunasubiri nini, lakini huwa tunahofu ya kupoteza ahadi tunayoisubiri ambayo kimsingi hatujaijua bado. Kimsingi, mambo tunayoyasumbukia katika maisha yetu ambayo ndiyo hasa hutufanya tuone kusubiri ni jambo gumu sana na linahitaji muda mrefu mno ni mambo ambayo sio msingi wa maisha yetu lakini huwa tunahofu ya kuyapoteza.
Mstari 25d “Maisha je! Si zaidi ya chakula, na mwili zaidi ya mavazi?”
MATHAYO 6:25-34
“Msijisumbue kwa neno lolote; bali katika kila neon kwa kusali na kuomba pamoja na kushukuru, haja zenu na zijulikane na Mungu. Na amani ya Mungu ipitayo akili zote itawahifadhi mioyo yenu na nia zenu katika Kristo Yesu - WAFILIPI 4:6-7
“Mtumaini Bwana kwa moyo wako wote, wala usizitegemee akili zako mwenyewe, katika njia zako zote mkiri yeye, naye atanyosha mapito yako. Usiwe mwenye hekima machoni pako; Mche Bwana, ukajiepushe na uovu -MITHALI 3:5-7
MAMBO 6 MUHIMU AMBAYO KUSUBIRI HUFANYA KATIKA MAISHA YETU
1.     Kusubiri hufunua nia zetu za ukweli.
Watu ambao hawana nia njema, iwe ni kwenye kazi, mahusiano nk. Hawawezi kusubiri muda mrefu kwasababu hawafurahishwi kuwa committed kusubiri jambo litokee, lakini hufurahishwa na hutamani kuona matokeo ya haraka
Mwanzo 11:1-6, inaeleza vema. Wale wajenga mnara walipokuwa na nia ya kwenda kinyume na ahadi ya Mungu kuwatawanya juu ya dunia nzima, waliona hapana haja ya kuisubiri hiyo ahadi hivyo wakajenga mnara ili wasitawanywe, wajifanyie kumbukumbu lao. Lakini walipoanza kujenga ni kana kwamba walikuwa na nia nzuri ya kufika juu kabisa mbinguni lakini wakati, ulielezea nia yao.
Watu wenye nia njema, husubiri.
2.     Huzaa moyo wa shukrani
Kitabu cha Yohana 9:1-41, utaona ni kwa kiasi gani huyu kipofu tangu kuzaliwa alivyokuwa na furaha na kiwango kikubwa cha shukrani, mara baada ya Yesu kumponya. Muda aliotumia katika kuamini na kuisubiria ahadi, ulibeba ukubwa wa shukrani yake.
Wengi hatuna mioyo ya shukrani kwasababu zile nyakati ambazo ilitakiwa tumsubiri Mungu afanye, sisi tulirush na kufanya wenyewe, tunapojipatia kina Ishamel kama Abram, hatuwezi kuwa na moyo wa kushukuru maana si mwana wa ahadi iliyo tarajiwa.
Hivyo, kusubiri, huzaa moyo wa shukrani kwa yale ambayo Mungu ametimiza

3.     Huimarisha Imani
“Wapenzi, sasa tu wana wa Mungu, wala haijadhihirika bado tutakavyokuwa; lakini, twajua ya kuwa, atakapo dhihirishwa tutafanana naye; kwa maana tutamuona kama alivyo. Na kila mwenye matumaini haya katika yeye, hujitakasa kama yeye alivyo mtakatifu.
1YOHANA 3:2-3
Huu ndio hasa msingi wa Imani yetu. Hatutakiwi kuchoka kusubiri, maana mbali na ahadi za kubarikiwa na kuwa vichwa tunazozingojea, ipo ahadi kuu zaidi ambayo ndiyo msingi wa Imani yetu, kudhihirishwa kwa Mwana wa Mungu ili tumfanane. Lakini, katika kusubiri ahadi hii, lazima tukubali kuuishi kana kwamba imekuwa, tuishi kwa utakatifu kama yeye alivyo.
4.     Hubadili tabia zetu
“Ilikuwa hapo Farao alipokwisha kuwaacha watu hao waende zao, Mungu hakuwaongoza kwa njia ya nchi ya Wafilisti, ijapokuwa ilikuwa ni ya karibu; Maana Mungu alisema, Wasije wakaghairi watu hawa hapo watakapo kutana na vita, na kurudi Misri.”
KUTOKA 13:17
Ilitakiwa Israeli wazungushwe na kusubiri sana jangwani, kwa muda wa miaka 40 ili Mungu abadili tabia zao. Kama asingewafanya wasubiri, akawaruhusu wapiti kwa njia fupi, wangekutana na vita, wasingekuwa mahodari na majasiri kupambana hadi mwish. Lakini Mungu aliwazungusha ili kutoa roho ya woga, na athari ya utumwa ndani yao ili wawe mahodari.
5.     Huimarisha ushirika na Mungu
Baadhi ya  mahusiano imara na ya kweli  tuliyo nayo, ni kwasababu ya mmoja wa rafiki kuweza kusimama imara na kwa ukaribu sana, katika nyakati ngumu ambazo tuliwahi kupitia.
Tunajifunza kuhusiana na watu wakuu katika maandiko ambao walitakiwa kusubiri ahadi za Bwana kutimia kwao kwasababu suala zima la kusubiri ahadi halikuwa ni mpango wa haraka haraka wa kusubiri siku kadhaa na kupata waliyosubiri lakini lakini walihitaji kwanza kukaa katika ushirika na Mungu kwa namna kubwa sana hata kama ingegharimu maisha yao yote.
Daudi, kwa mfano, alitawazwa kuwa mfalme wa Israel akiwa na umri mdogo tuu, lakini ilitakiwa asubiri tena akiwa katika mahusiano imara na Mungu, miaka mingi sana mbele ili kukalia kiti cha ufalme. Yusufu pia, alikuwa na ndoto lakini ilimgharimu mambo mengi sana hadi ndoto kutimia, na kwa wakati wote wa kusubiri ndoto itimie, alitakiwa kuishi maisha yanayo akisi uimara wa ushirika wake na Mungu
Hivyo katika kusubiri, si mbaya sana kama utaitazama sana ahadi, lakini ni nzuri zaidi kama utamtazama mtoa ahadi na kujenga ushirika nae.
6.     Hutengeneza uvumulivu
Mungu anapoiangalia ahadi aliyokuahidi, haioni kuwa ni kubwa na muhimu sana kama kukusubirisha ili akutengenezee misuli ya uvumilivu. Na hili, lifanye hata shuhuda zetu zibadilike. Tunapokuwa tumemwamini Mungu katika ahadi flani kubwa, na ikatokea hajafanya kwa wakati tulio tegemea, tusikatishwe tama. Tumshukuru maana ametutengenezea misuli ya uvumilivu jambo ambalo ni kubwa kuliko ahadi iliyo ahidiwa.
Ibrahimu, alikaa muda mrefu sana kumngojea Isaka. Na alipokuja Isaka, Ibrahim alikuwa tayari na misuli mikubwa sana iliyotokana na kusubiri, kiasi ambacho hata alipoambiwa akubali kwa makusudi kuipoteza tena ahadi aliyoingoja miaka mingi (kumtoa Isaka sadaka), hakusita.



TAG PENUEL LUHANGA – JABA
©Sam Gripper 2018, Assistant Pastor
0657 670972
Unknown
Unknown

This is a short biography of the post author. Maecenas nec odio et ante tincidunt tempus donec vitae sapien ut libero venenatis faucibus nullam quis ante maecenas nec odio et ante tincidunt tempus donec.

No comments:

Post a Comment