MLANGO


MLANGO

By Pastor Sam Gripper

4th March 2018

10 Wala msinung’unike kama wengine wao walivyonung’unika wakaharibiwa na mharibu.  11 Basi mambo hayo yaliwapata wao kwa jinsi ya mifano, yakaandikwa ili kutuonya sisi, tuliofikiliwa na miisho ya zamani. 12 Kwa hiyo anayejidhania kuwa amesimama aangalie asianguke. 13 Jaribu halikuwapata ninyi, isipokuwa lililokawaida ya wanadamu; ila Mungu ni mwaminifu; ambaye hatawaacha mjaribiwe kupita mwezavyo; lakini pamoja na lile jaribu atafanya na mlango wa kutokea  ili mweze kustahimili

1KORINTHO 10:10-13

Imenipasa kunukuu kuanzia mstari wa 10 ingawa mstari lengwa zaidi ni ule wa 13 ambao unazungumza mambo makuu manne nitakayo yazungumzia katika somo hili. Mambo hayo ni jaribu lililo kawaida ya wanadamu, uaminifu wa Mungu, mlango wa kutokea na kustahimili.

Tukianzia sura ya 10 na mstari wa 1 kabisa, tunaanza kuona Paul akifunua fundisho lililokuwa chini au nyuma ya tendo la wana wa Israel kutolewa Misri, kupitishwa katika bahari ya Sham na kuongozwa jangwani.

Tendo lao la kuongozwa na wingu na kupitishwa katikati ya bahari Paul analizungumzia kuwa ni fundisho juu ya ubatizo, kwamba Taifa lilibatizwa ili kuwa mali ya Musa, Mwamba/nguzo ambayo ilionekana ikiwaongoza mara zote, na mara yingine hata kutoa maji kwaajili yao, Paul anaufunua kama ni Kristo. Lakini mstari wa 6 Paul anazungumza kuwa mambo haya yote yalitokea kwa namna ya mfano (kivuli ili kuakisi maisha ya Kristo na kanisa). Mstari wa 11 pia Paul anarudia kusema kuwa haya mambo yalikuwa ni kivuli na yakaandikwa ili sisi kama kanisa tujifunze na tuonywe kwa hayo.

Kila mmoja anapoingia katika shida, au jaribu la aina yoyote jambo la kwanza kabisa ambalo anatamani litokee, ni mlango wa kutoka katika jaribu hilo. Na hapa, ninapozungumza kuhusiana na jaribu, nazungumzia yale ambayo Mungu huwa anatupa kuzipima na kuziinua Imani zetu nay ale ambayo yanatokana na tama zetu na shetani anayatumia kututoa katika mstari ambao Mungu amekusudia tuwe.

“Mtu ajaribiwapo asiseme ninajaribiwa na Mungu; maana Mungu hawezi kujaribiwa na maovu; wala yeye mwenyewe hamjaribu mtu. Lakini kila mmoja hujaribiwa na tama yake mwenyewe, huku akivutwa na kudanganywa”

YAKOBO 1:13-14

[Kwa kibali cha Mngu nitakuja siku moja kuandika juu ya utofauti wa majaribu (trials) yanayoletwa na Mungu na majaribu (temptation) yanayotumiwa na shetani kutokana na tama zetu]

Lakini katika aina yoyote ya jaribu alilonalo mtu, huwa jambo la kwanza ambalo analihitaji, ni mlango wa kutoea. Nitasimamia katika andiko letu la kwanza kutoka 1Korintho 10:13 kueleza mambo kadhaa kuhusu mlango wa kutokea.

1.     Kila jaribu lina mlango wa kutokea

Inaweza ikawa ni kauli nyepesi sana, lakini namwomba Mungu akufunulie maarifa ili usiisome kwa wepesi. Jaribu, shida au tatizo huweza kuambatana na kuchukiwa, kudharauliwa, kutengwa, kunyoshewa vidole, maumivu, kujidharau, kupingwa, kuwekewa kila aina ya vizuizi, lakini pia huambatana na mlango wa kutokea.

Mungu anapolileta au kuruhusu shida au jaribu kwako, hulileta na kuliruhusu kama kifurushi kamili (a complete package). Na moja kati ya vitu vinavyofanya kifurushi hicho kiwe kamili, mbali na shida na maumivu vinavyo ambatana na tatizo hilo,  ni uwepo wa mlango wa kutokea. Kwa lugha nyingine ni kwamba kama ambavyo hakuna jaribu lisilozaa maumivu, ndivyo ambavyo hakuna jaribu lisiloletwa na mlango wake.



2.     Kufunguliwa kwa mlango, ni jambo dogo kuliko mafunzo uyapatayo kanla mlango haujafunguliwa

Kila mmoja anayepita katika aina yoyote ya shida huwa na fikra ya kwamba jambo kubwa na muhiu kuliko yote ni kufunguliwa mlango ili atoke katika shida hiyo. Kufunguliwa mlango ni jambo dogo sana kuliko ukubwa wa maarifa unayotakiwa kuyapata ndani ya gereza na kabla mlango haujafunguka.

Lengo la Mungu kuruhusu upite katika eneo flani gumu, sio kukuacha tu na baadaye kukufungulia mlango utoke kiurahisi. Yale atakayokuwa akikufundisha ndani ya gereza na kabla mlango haujafunguka ndio hutafsiri wakati wa mlango wako kufunguka. Hivyo, hakuna mlango kufunguka kama hakuna misuri iliyotengenezwa.

Katika mstari 13, wa andiko letu kuu maandiko yanasema Mungu atafanya mlango wa kutokea ili tuweze kustahimili. Maana yake kiwango cha ustahimilivu kitaamua wakati wa mlango wako kufunguka na kitaamua aina maisha utakayoanza kuyaishi ukiwa nje ya gereza.

3.     Sio kila mlango unaofunguka mbele yako ni kwaajil yako

Inaweza kuwa ni kauli tata na yenye kushtusha lakini nina uhakika juu ya hili. Tunaposoma habari za Abramu katika kitabu cha Mwanzo 16:1-16, tunaona matokeo ya Sarai kumlazimisha Abram kuingia katika mlango ulioonekana kana kwamba ni kwaajili yake kupita na kumbe haukuwa wake.

Sara hakuwa na uwezo wa kuzaa ingawa tayari Mungu alimuahidi Ibrahim kujitwalia uzao. Sara pasipo nia mbaya, akauona mlango mwingine kwaajili yao kupata uzao ambao ulikuwa ni Abram kumwingilia kimwili mjakazi. Ni jambo ambalo halikuufunga mlango wa Mungu, lakini lilizaa chuki kubwa katika familia hata leo hii chuki hii inaendelea kati ya Waarabu na Waisrael.

Kila  mtu anamlango wake kulingana na kifurushi cha jaribu analopitia. Mlango wa jaribu langu, unaweza usiwe ni njia ya kukutoa wewe katika jaribu lako, hata kama sote tunapitia katika matatizo au hali sawa. Jifunze kumsiilza Mungu na kungoja ruhusa yake kwa kila njia anayoifungua mbele yako

4.     Maneno unayozungumza ndani ya jaribu/tatizo na mara baada ya kutoka katika jaribu yanatafsiri wewe ni nani na moyo wako mbele za Mungu.

Katika sura ya 10 mstari wa 1 wa Wakorintho wa 2, Paul anaeleza ni kwa namna gani Mungu aliliongoza Taifa la Israel nyakati zote kutoka Misri hadi kuelekea Kanani, na ni kwa namna gani walianguka katika ibada za sanamu wakiwa njiani, kwakuwa tuu hawakuona Mungu kama anampango nao na wakamlaumu hata Musa kwa kuwatoa Misri.

Ukiwa ndani ya jaribu, unaongea nini kuhusiana na wewe mwenyewe? Unaongea nini uhusiana na Mungu? Unaongea nini kuhusiana na watu ambao wapo kwenye hali kama yako, au wamekuzidi, au wamepungua kuliko wewe? Chochote unachowaza na kuzungumza juu ya mabo hayo kitatafsiri ushindi wako na kitakutafsiri mbele za Mungu pia.

Ayubu siku zote aliishi na mke wake na hakuwahi pengine kujua kuwa mke wake ni mpumbavu kama wanawake wengine, hadi kipindi ambacho Ayubu alipitia magumu, na Mke wake akataka Ayubu aongee vibaya kuhusu Mungu. Ashukuriwe Mungu neno kuu moja ambalo Ayubu alikuwa akizungumza ni “Ninajua mtetezi wangu yu hai”

Hivyo tatizo au jaribu lolote linalokukuta, sio geni ni kitu ambacho kama hakikutokea katika namna ya mifano kutoka kwa wazazi wetu walioishi kabla yetu, basi kitatokea katika namna ya mfano kwa kizazi kijacho mbele yako. Kwamba kizazi kijacho kitatakiwa kujifunza namna ulivyomtumaini Mungu katika  hilo unalopitishwa na namna ulivyotoka. Na lengo la Mungu, sio kukutoa katika jaribu au shida na akakulinda usiingie katika hali hiyo tena.. lakini lengo lake ni kutengeneza nguvu na ustahimilivu ndani yako, vitakavyo amua na kukupa ushindi kila mara ukutanapo na jaribu au hali ngumu zaidi.

Umebarikiwa, SHALOM!!



©Pastor Sam Gripper

TOTAL TRANSFORMATION YOUTH MINISTRY/TAG PENUEL LUHANGA
0657670972


Unknown
Unknown

This is a short biography of the post author. Maecenas nec odio et ante tincidunt tempus donec vitae sapien ut libero venenatis faucibus nullam quis ante maecenas nec odio et ante tincidunt tempus donec.

No comments:

Post a Comment