SHUKRANI


SHUKRANI

By Pastor Sam Gripper

18th  Feb 2018



Marko 11:24

“Kwa sababu hiyo nawaambia, Yoyote myaombayo mkisali aminini ya kwamba mnayapokea, nayo yatakuwa yenu.”

Tunaanza kwa andiko hili ambalo ndilo hasa linafunua msingi wa shukrani. Pengine hatukuwahi kuona au hatuwezi kuona uhusiano uliopo kati ya mambo haya matatu, imani, maombi na shukrani. Na huenda katika somo hili, nikaegemea sana katika haya mawili ya kwanza kuliko katika shukrani yenyewe maana hayo ndiyo hasa hujenga msingi wa shukrani.

Kitabu cha Marko hapo juu kinaonesha msingi wa kupokea kitu kuwa haupo katika kuwa na kile kitu tayari kama majibu ya maombi, lakini upo katika kuanza kukimiliki kile kitu kabla hata hakijadhihirika kama jibu la maombi yako. Hivyo unapoenda kumuomba Mungu juu ya kitu ambacho ni hitaji lako, lazima uamini kuwa hicho kitu umekipokea tayari. Ukilijua hilo, utaepuka kuomba maombi ya lawama, badala yake utamshukuru maana katika namna ya Imani, tayari unayo majibu ya unachoenda kuomba.

Na hapo ndipo mahali ambapo shukrani, imani na maombi hukutana na mambo haya matatu yote hutegemeana. Tunaomba ili tupate mahitaji yetu, na mahitaji yote tunayoomba au hata tusiyo yaomba huwa tunayapokea kulingana na kiasi gani tumeamini kuwa mambo hayo ni yetu tayari. Hii imani hutupa nguvu ya kumiliki na kushukuru sio tuu kwa yale yaliyodhihirika kwetu, lakini juu hata ya yale ambayo bado hayajadhihirika na tunamuamini Mungu kuwa yatadhihirika.





Waebrania 11:5-6

“Kwa imani Henoko alihamishwa, asije akaona mauti, wala hakuonekana, kwa sababu Mungu alimhamisha; maana kabla ya kuhamishwa alikuwa ameshuhudiwa kwamba amempendeza Mungu.

Lakini pasipo Imani haiwezekani kumpendeza; kwa maana mtu amwendeaye Mungu lazima aamini yeye yuko na huwapa thawabu wale wamtafutao.”

Katika andiko hilo hapo juu, yapo mambo ambayo nataka tuyaone lakini zaidi namuomba Mungu uamini na mimi juu ya mambo hayo. Maandiko yanaanza kueleza katika kitabu cha Mwanzo 5:22 kuwa, “Henoko akaenda pamoja na Mungu, naye akatoweka maana Mungu alimtwaa.” Katika kitabu cha Waebrania hapo juu, maandiko yanatufunulia nini ambacho Mwanzo haikutufunulia kwa upana.

Maandiko yanaanza kusema, “kwa imani Henoko alihamishwa”. Hivyo namna pekee ambayo Henoko aliweza kuishi na Mungu na kutembea naye, ilikuwa ni namna ya kuanza kwanza kumuamini. Nataka niamini kuwa maandiko hayamaanishi kuwa Henoko alitembea na Mungu kama mtu awezavyo kushikana mkono na jirani yake kisha wakatembea. Bali, kutembea na Mungu hapa, ni kuishi maisha yanayompendeza Mungu.

Nataka niamini pia kuwa imani ya Henoko ilimpeleka katika point ya kuwa na njia zake binafsi za kumruhusu Mungu ajidhihirishe kwake, jambo lililomfanya pia Mungu ajiridhishe kwa Henoko kitofauti sana kiasi cha yeye Mungu kuamua kumchukua kinyume na utaratibu wa kifo aliouweka baada ya anguko.

Kwakuwa kila siku, Henoko alikuwa na njia binafsi (tofauti na watu wengine) na thabiti zilizomfanya Mungu adhihirike kwake, maana yake aliruhusu akili yake imuone Mungu akiwa halisi katika kila eneo la maisha yake. Na kwa namna hii nataka niamini kuwa hata namna yake ya maombi na mtazamo juu ya mambo mbalimbali haikuwa ya kawaida.



Ni rahisi sana kumshukuru Mungu kama utakuwa umeiruhusu akili yako imuone Mungu akiwa halisi kwako kila siku na katika kila jambo. Hata maombi yako hayatakuwa ya lawama badala yake ya kushukuru maana umeruhusu imani ikupeleke mahali flani pakubwa na muhimu sana pa kumuona Mungu akiwa halisi katika kila jambo.

Ebrania 11:11

Kwa imani hata Sara mwenyewe alipokea uwezo wa kuwa na mimba; alipokuwa amepita wakati wake kwakuwa alimhesabu yeye aliyeahidi kuwa mwaminifu”

Ebrania 11:17, 19

“Kwa imani Ibrahim alipojaribiwa, akamtoa Isaka awe dhabihu; na yeye aliyezipokea hizo ahadi alikuwa akimtoa mwanawe mzaliwa pekee

Akihesabu ya kuwa Mungu aweza kumfufua hata kutoka kuzimu; akampata tena tuko huko kwa mfano.

Wakati ambao Sara alipokea uwezo wa kupata ujauzito, haukuwa wakati ambao tayari yu mjamzito. Ulikuwa ni ule wakati ambao alikuwa katika hali ya kushindwa kuwa mjamzito. Lakini kwa njia ya imani alianza kumiliki jibu la maombi yake katika hali ya upungufu aliokuwa nao. Hii yote ilikuwa ni kwasababu aliamua kumuona Mungu yu mwaminifu (mkweli kwa jina lake na kwa ahadi yake mwenyewe).

Ni point gani hasa ambayo unaanza kumshukuru Mungu? Unamshukuru Mungu mara baada ya kuwa na muujiza wako mkononi au unashukuru Mungu wakati ambao hata dalili ya kuwa na muujiza wako haipo? Asilimia kubwa ya watu wanaotoa sadaka ya shukrani katika makanisa, huwa wanatoa mara baada ya kupokea waliyokuwa wanatarajia, jambo ambalo sio baya. Lakini lazima tukubali imani yetu ituchukue na kutupeleka katika point ya kuweza kumshukuru Mungu hata kabla tunayotarajia hayajadhihirika katika namna ya mwili.



Ibrahim, alitoa karibia maisha yake yote kuisubiri ahadi ya kumpata Isaka. Lakini mara baada ya kumpata, anatakiwa afanye maamuzi ya dakika isiyozidi moja kutimiza juu ya agizo ambalo Mungu alimpa. Katika Ebrania 11:11 tumeona kuwa Sarai alipokea uwezo wa kupata mimba kabla hajawa na huo uwezo, kwakuwa alimhesabu Mungu kuwa ni mwaminifu. Hapa Ibrahim hasiti kumtoa Isaka kama sadaka, maana alimhesabu Mungu kuwa anaweza kumfufua tena.

Hii haina tofauti na kwa Henoko. Alikuwa na nja zake binafsi ambazo kupitia alimuona Mungu akidhihirika katika namna kubwa katika maisha yake. Ibrahim alipokuwa akimtoa Isaka, ndani kabisa ya fahamu zake za kiimani aliamua kumpokea tena Isaka kama mfano (he received him in a figure). Hivyo alikuwa tayari kumpoteza Isaka katika mwili ili arudi kummiliki tena katika mfano kama alivyokuwa akifanya wakati anasubiri ahadi ya kuwa na Isaka itimizwe.

Mtu mwenye macho na misuli ya namna hii ya imani neno shukrani kwake huwa ni zaidi ya kusema asante.

Unahesabu nini/unamhesabuje Mungu:-

¨ Mungu anaporuhusu upite katika nyakati ngumu ambazo unapoteza kila ulichonacho?

¨ Unapotoa nguvu yako kubwa katika kuomba na kuamini juu ya hitaji lako, na majibu yakawa tofauti na ulivyotamani wewe kwa akili zako?

¨ Unapokuwa umepata ahadi kinyume na ulizo tarajia?

¨ Unapokuwa umepata kila unachotarajia?

Zaburi 100:4-5

“Ingieni malangoni mwake kwa kushukuru; nyuani mwake kwa kusifu, Mshukuruni lihiidini jina lake; kwakuwa Bwana ndiye mwema, Rehema zake ni za milele; Na uaminifu wake vizazi na vizazi”





Katika kila hali na kila jambo tunalopitia, lazima tufahamu kuwa halimbadilishi Mungu. Na tunatakiwa kumshukuru pasipo kujali lolote tunalopita kwasababu hata katika madhaifu yetu shida zetu, vifungo, kupungukiwa au chochote yeye bado ni Mungu. Na namna pekee ya kusogelea mahali alipo ni kuamini kuwa yeye yupo (Waebrania 11:6) na kushukuru kama ambavyo Zaburi imezungumza.













©Pastor Sam Gripper

TAG PENUEL LUHANGA & TOTAL TRANSFORMATION

0657670972



Unknown
Unknown

This is a short biography of the post author. Maecenas nec odio et ante tincidunt tempus donec vitae sapien ut libero venenatis faucibus nullam quis ante maecenas nec odio et ante tincidunt tempus donec.

No comments:

Post a Comment